PASTA mmoja kutoka eneo la Ukunda kaunti ya Kwale amewaondolea Wakenya hofu dhidi ya uwezekano wa kunyesha kwa mvua kubwa ya El Nino kuanzia Oktoba.
Geoffrey Mwariga ambaye pia ni mmiliki wa kituo cha mayatima cha Born Again Children eneo hilo anadai kuisitisha mvua hiyo kupitia maombi aliyofanya mnao Septemba 13, 2015.
Akiongea na waandishi wa habari nyumbani kwake, Bw Mwariga alisema kuwa mwenyezi Mungu alimpatia uwezo huo ili kurudisha imani wa waumini kwa viongozi wa kidini.
Aidha alidokeza kuwa alichukua hatua ya kusitisha mvua hiyo kwa heshima ya Mungu kwa sababu aliona ya kwamba serikali haina uwezo wa kuzuia uharibifu wake.
“Ningependa kuwaondolea wakenya hofu na serikali kwa ujumla ya kuwa hakutokuwa na El-nino kama vile ilivyotangazwa na idara ya utabiri wa hali ya hewa,” akasema Bw Mwariga.
Bw Mwariga alieleza kuwa iwapo mvua hiyo ingelinyesha basi ingelileta maafa makubwa zaidi ya wale ambao wamefariki katika ajali za barabarani, mikasa ya moto na kadhalika.
Aliongeza kuwa sababu kuu ambayo ilipelekea kukubaliwa kwa maombi yake ni msimamo wa Rais Uhuru Kenyatta dhidi ya kupinga ushoga na usagaji humu nchini.
“Wakati ambapo kiongozi wa nchi aliposimama na kupinga ushoga hapo ndio El-nino ilipotea kwa sababu ilibainika kuwa haungi mkono mambo ya kishetani,” akasema pasta huyo.
Pasta huyo alisema kuwa mvua hiyo haipaswi kuchukuliwa kama jambo la kawaida kwa sababu inatokana na roho ya uharibifu ambayo lengo lake kuu ni kusababisha uangamifu.
Nguvu za maombi
Alikariri kuwa kama vile viongozi wa kidini walivyofanikiwa kuzuia maafa yaliyokuwa yakishuhudiwa kila mwezi, kupitia maombi mvua hiyo pia imezuiliwa.
“El-nino inapokuja huwa kuna laana fulani ambayo imesababisha na njia moja ya kuondoa laani hiyo ni kujielekeza mbele ya Mungu na kutubia dhambi zetu,” akasema Bw Mwariga.
Wakati huo huo Bw Mwariga aliwahisi viongozi wengine wa kidini ambao wametwikwa jukumu la kuombea nchi wachukulie tahadhari zote zinazotolewa kwa uzito zaidi.
Alisema kuwa iwapo tukio lolote baya linaweza kujitokeza na kuleta maafa humu nchini ni ishara tosha wale ambao wamepatiwa mamlaka hawawajibikii majukumu yao.
“Bibilia inasema tukiwa na imani ndogo kama chembe cha haradai tutauambia ulima ng’oka tupwa baharini kwa hivyo sihitaji imani kubwa kusimamisha El-nino,” akasema Bw Mwariga.